Baadhi ya wazee wameitaka serikali iwatambue wazee kwamba wapo, pia iwahudumie hasa katika sera ya matibabu bure kwa wazee maana wakati mwingine hukosa dawa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya
Na Adelinus Banenwa
Imeelezwa kuwa wazee wawili (2)hadi watatu (3) kati ya wazee kumi (10) halmashauri ya mji wa Bunda hufanyiwa ukatili mbalimbali katika jamii na familia.
Hayo yamesemwa leo na afisa ustawi wa jamii halmashauri ya mji wa Bunda mkoani Mara Waryoba Juma ambapo amesema takwimu hizo siyo nzuri lakini pia siyo mbaya ukilinganisha na maeneo mengine nchini.

Waryoba amesema ukatili wanaokutana nao wazee ni pamoja na kubaguliwa, kunyanyaswa, kutosikilizwa na wakati mwingine wazee wanapigwa matukio ambayo matukio haya yanagawanyika katika makundi mawili ya unyanyasaji ambayo ni kimwili na kisaikolojia.
Waryoba ameyasema hayo katika kikao kilichowakutanisha wazee kutoka mitaa ya kata ya Sazira walipokuta na viongozi wa baraza la ushauri la wazee halmashauri ya mji wa Bunda.
Kwa upande wao baadhi ya wazee wameitaka serikali iwatambue wazee na kwamba wapo pia iwahudumie hasa katika sera ya matibabu bure kwa wazee maana wakati mwingine hukosa dawa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya pia watoto wao kushindwa kuwalea na badala yake huwarundikia wajukuu nyumbani bila utaratibu.

Naye Machael Kweka ambaye ni mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Bunda na diwani wa kata ya Sazira ameiomba serikali kuleta mpango wa kulipa pensheni kwa wazee wa Tanzania bara kama inavyofanyika huko Zanzibar na lingine watoto wenye kazi kuhakikisha wanawakatia bima za matibabu wazee wao.