- Mazingira FM

Mazingira Fm Live

Breaking News

Thursday, 27 February 2025

 

Kampeni ya chakula shuleni yapelekea shule 11 bunda tc kufuta daraja 0

27 February 2025, 

Mhe Mbunge wa jimbo la Bunda mjini Mhe Robert Chacha Maboto akiwa katika moja ya shule za sekondari Bunda mjini katika ziara yake ya kuhamasisha chakula shuleni.

Yapo mabadiliko makubwa ya kitaaluma tangu sera ya wanafunzi kupata chakula shuleni ambapo kati shule 17 za sekondari za halmashauri ya mji wa Bunda shule 11 zimefanikiwa kufuta daraja sifuri kwa matokeo kidato cha nne.

Na Adelinus Banenwa

Mbunge wa jimbo la Bunda mjini Mhe Robert Chacha Maboto amewataka wazazi wa wanafunzi katika jimbo la Bunda mjini kufanya kila linalowezekana kuhakikisha wanachanga chakula cha wanafunzi shuleni kama wanahitaji matokeo mazuri kwa watoto wao.

Kauli hiyo ameitoa leo tarehe 26 Feb 2025 katika siku ya tatu ya ziara yake iliyokuwa inalenga kuhamasisha chakula shuleni huku katika siku hizo tatu Mhe mbunge ametembelea jumla ya shule za sekondari 16.

Mhe Robert Chacha Maboto mbunge wa jimbo la Bunda mjini akisalimiana na moja ya wanafunzi shule ya sekondari Nyiendo alipofika katika ziara yake ya kuhamasisha chakula mashuleni

Mhe Maboto amesema hakuna ambaye hafahamu juu ya ugumu wa maisha lakini suala la chakula shuleni ni jambo la mzazi kuelewa na kuamua endapo anataka matokeo mazuri ya mtoto hasa kitaaluma hivyo kila mzazi anao wajibu wa kitimiza majukumu yake.

Sauti ya Mhe Robert Chacha Maboto mbunge jimbo la Bunda mjini

Afisa lishe halmashauri ya mji wa Bunda Bi Lucy Erasto Mwalwayo amesema yapo madhara mbalimbali ya muda mrefu ambayo yatampata mtoto endapo atakaa muda mrefu bila kupata chakula shuleni ambapo amesema madhara hayo ni pamoja na kuwa na tabia ya kuishiwa damu pindi atakapofikia kipindi cha kuzaa kwa watoto wa kike, upungufu wa nguvu za kiume kwa watoto wa kiume, vidonda sugu vya tumbo pamoja na kupata saratani ya utumbo.

Sauti ya afisa lishe halmashauri ya mji wa Bunda Bi Lucy Erasto Mwalwayo
Mhe Robert Chacha Maboto mbunge wa jimbo la Bunda mjini kwenye picha ya pamoja na baadhi ya wanafunzi shule ya sekondari Bunda alipofika kuhamasisha uchangiaji wa chakula mashuleni

Kwa upande wake Sauda Mwakyembe kaimu afisa elimu sekondari kwa upande wa halmashauri ya mji wa Bunda amesema yapo mabadiliko makubwa ya kitaaluma tangu sera ya wanafunzi kupata chakula shuleni ambapo kwa matokeo ya kidato cha nne mwaka 2024 kwa shule zote 17 za sekondari za halmashauri ya mji wa Bunda shule 11 zimefanikiwa kufuta daraja sifuri kwa matokeo kidato cha nne.

Sauti ya Sauda Mwakyembe kaimu afisa elimu sekondari Bunda TC

Ikumbukwe katika ziara yake ya siku tatu aliyoifanya mbunge wa jimbo la Bunda mjini kwa jumla ya shule 16 za sekondari za Bunda mjini ametoa jumla ya magunia 65 ya mahindi na kilo 800 za maharage ikiwa ni kuunga mkono juhudi za wazazi kuchangia chakula cha wanafunzi shuleni ili kuongeza kiwango cha taaluma.

No comments:

Post a Comment